Kwa mujibu wa Kitengo cha tarjama cha Shirika la Habari la Hawza, ofisi hiyo ilisimamiwa na Amira Elghawaby, ambaye alikuwa na jukumu muhimu katika kuchunguza vikwazo na changamoto za kiuchumi zinazowakabili Waislamu, kutoa ushauri kwa taasisi za serikali, kuandaa programu za mafunzo ya kupambana na chuki dhidi ya Uislamu, na kuunga mkono tafiti kuhusu namna vyombo vya habari vinavyoripoti uhalifu wa chuki dhidi ya Waislamu.
Tathmini zinaonesha kwamba takribani robo tatu ya wanawake Waislamu katika jimbo la Quebec, Canada, wamefikiria kuondoka katika jimbo hilo kutokana na ubaguzi na manyanyaso. Hali hii inatokea wakati baadhi ya wanasiasa wa Canada wakiendelea kukanusha kuwepo kwa chuki dhidi ya Uislamu katika jimbo hilo.
Bi. Elghawaby amejitahidi kuibua waziwazi katika fikra za umma wa Canada suala la chuki dhidi ya Uislamu na kubainisha madhara yake katika jamii nzima. Hata hivyo juhudi zake zimekabiliwa na ukosoaji mkali, ikiwemo shutuma za kujaribu kuleta mgawanyiko nchini au kueneza propaganda za chuki dhidi ya Wayahudi.
Aidha, uamuzi wa Waziri Mkuu Mark Carney wa kuifunga ofisi hiyo umeibua ukosoaji mkali, hasa kufuatia kauli za awali za Pierre Poilievre, kiongozi wa Chama cha Conservative cha Canada, ambaye aliwahi kuitaja misimamo hiyo kuwa “isiyo na manufaa”.
Watetezi wa kufunguliwa tena kwa ofisi hiyo wanasema kwamba; suala hili linahitaji kuongezwa kwa rasilimali na dhamira ya kisiasa katika kupambana na chuki dhidi ya Uislamu, na wanaonya kwamba bila kuwepo kwa mifumo ya uwajibikaji, vurugu dhidi ya Waislamu zitaendelea kubaki kuwa hatari isiyoonekana.
Chanzo: Policy Options
Maoni yako